| |
NJIA
YA KWENYE KIFO YENYE MAVUMBI
Asubuhi
ya Jumapili ya Juma lililopita, Mahmoud
Shawara, kibarua, alipanda nyumbu wake na
akatoka nyumbani kwake katika kijiji cha
Nuaman kwenda kutafuta kazi katika kijiji
cha jirani cha Umm Touba. Majira ya kama
saa 3.00 asubuhi alikamatwa na Polisi wa
kituo cha Mpakani ambacho kinawaweka kizuizini
wafanyakazi ambao hawana kibali cha kuingia
Israel kila asubuhi.
Askari hao wa mpakani walimuamuru Shawara
kuingia kwenye gari lao aina ya Jeep. Yeye
akakataa. Hakutaka kumuacha nyumbu wake
bila uangalizi. Majira ya saa 3:30 asubuhi
kaka yake alimuona kwa mara ya mwisho akiwa
mwenye afya na timamu. Mnamo saa 10 jioni,
mkazi wa Umm Touba aitwaye Mohammed Hamadani
alimuona nyumbu akienda shoti kuelekea hapo
kijijini na akiwa anaburuza kitu fulani
nyuma yake. Kutoka mbali kidogo Mohammed
Hamadani alifikiria ingeweza kuwa chuma
kilichochakaa. Jinsi farasi yule alivyozidi
kusogea karibu, Mohammed Hamadani aliweza
kuona kwamba alikuwa anaburuza mtu aliyejeruhiwa
kapondwa-pondwa. Nyumbu yule, yeye anasema,
alikuwa anakwenda shoti kushuka kilima na
alionekana aliyetishwa. Alimsimamisha mnyama
huyo na kisha akagundua kwamba yule mtu
aliyekuwa akiburuzwa kwenye ardhi alikuwa
ni Mahmoud Shawara, kutoka kijiji cha jirani
ambaye alikuwa anamtambua vizuri. Mkono
wa kushoto wa Shawara ulikuwa umefungwa
kwenye shingo ya nyumbu huyo. Alikuwa hanafahamu
na akipumua kwa shida. Fuvu lake na uso
vilikuwa vimepondeka upande wa kushoto na
alikuwa akitoka damu. Aliweza kutamka maneno
machache yaliyokatika katika, yasiyoeleweka
vizuri au sehemu za maneno kisha akafunga
pumzi.
Hamadani alimfungua kamba Shawara, akamlaza
chini na akamminya kifuani mwake ili kumrudishia
pumzi yake. Kisha akaita gari la wagonjwa
kutoka kwenye kliniki ya kituo cha afya
cha shirika la matengenezo la Mauhedet kijijini
hapo. Shawara alipelekwa kwenye kituo cha
afya huko Ein Kerem, Jerusalem ambako alilazwa
katika sehemu ya tiba ya Nyurolojia ya kitengo
cha wagonjwa mahututi. Mwishon mwa wiki,
ambamo hakupata kurudiwa na fahamu, Shawara
alifariki kutokana na majeraha yake. Alikuwa
na umri wa miaka 43, mfanyakazi na baba
wa watoto tisa, aliyekuwa amekwenda kutafuta
kazi katika kijiji cha jirani.
Shawara aliuawa vipi? Je, Polisi wa mpakani
walimtesa kimwili na kumfunga kwenye mnyama
kisha wakamtishia mnyama huyo akimbie na
kusababisha kifo chake kutokana na mapigo
kwenye kichwa kwenye mawe vile mnyama huyo
alivyokuwa akienda mrama kushuka kilima
hicho? Je, alipigwa kisha kafungwa kwenye
nyumbu huyo, ambaye baadae aliswagwa kuchukua
njia yake? Au Idara ya upelelezi ya Polisi
wa Wizara ya Sheria wako sahihi katika kudai
kwamba hii ilikuwa ni ajali ya upandaji
wa nyumbu – Shawara alijifunga mwenyewe
kwenye nyumbu, akaanguka toka juu yake na
akaumia vibaya sana.
Watu hapo
Nuaman walituambia juma hili kwamba Polisi
hao wa mpakani kwa kawaida huwafunga kamba
watu ambao wamo ndani ya Israeli kinyume
cha sheria (shabahim) kwenye wanyama wao.
Tutataja ushahidi wa mfanyakazi mwingine
Mpalestina ambaye alifungwa kwenye punda
wake na Polisi wa mpakani majuma machache
yaliyopita kama alivyokuwa amelala chini
aridhini, uso ukiangalia chini na mikono
yake ikiwa imefungwa nyuma ya mgongo wake
na pande la mkaa mgongoni mwake likiwa limewekwa
hapo na Polisi wa mpakani. Katikati ya Nuaman
na Umm Touba, vijiji viwili vyenye amani
juu ya bonde la kustajabisha, ndipo lilipo
eneo hilo la kuburuzia.
Picha ya karibu ya tishio hilo: Uso wa yule
mtu aliyeuawa umepondwa. Mwili wa Shawara
umelala sakafuni nyumbani kwake, ukiwa umefunikwa
na bendera ya Palestina na shuka kutoka
kituo cha afya cha Shaare Zadek, Jerusalemu
(ingawaje alifia Hadassah). Nyumba hiyo
– jengo lisilo halali – haina
paa, isijekuwa ingebomolewa na Israeli.
Turubai la rangi ya buluu limefunika makazi
hayo kuyalinda dhidi ya hali ya hewa.
Ni wakati wa mchana, dakika chache kabla
ya shughuli za mazishi zianze, siku ya Jumapili
ya Juma hili. Mtu mmoja anaweka bendera
ya Hamas kwenye mwili wa marehemu,juu ya
ile bendera ya Palestina na lile shuka la
Shaare Zedek. Wanawake wa familia hiyo wanalia
visivyotulizika; yule binti mkubwa, Kauther,
24, yuko karibu kuzimia. Kabla mwili kutolewa
chumbani, ule uso, ukiwa umefunikwa isivyo
kawaida, ili kuficha yale majeraha. Gavana
wa Bethelehem, Salah Taamri, amesimama hapo
nje pamoja na watu maarufu wa hapo. Mazishi
yamezuiwa, magumu. Kuna ukelele mmoja tu
wa siasa kali Ewe Yahudi, Ewe Nguruwe, tutakukanyaga
chini ya miguu.
Wanakijiji hao wameshawishika kwamba Shawara
alikuwa ameuawa na Polisi wa mpakani. Lakini
pale jeep la Polisi wa mpakani inapojitokeza
ghafla katikati ya mazishi, kwa mtazamo
wa juujuu wa uchokozi, kule kuzuiwa kunadumishwa.
Hii ndio tabia ya hawa watu wa kilimani:
Wanashindwa kuongea na wenye wasiwasi sana.
Nuaman iko kwenye barabara ya wazi ya kwenda
Jerusalem, katikati ya Bethelehem na mji
mkuu wa Israel, mashariki ya ujirani wa
Har Homa katika sehemu ambayo ule ukuta
unaotenganisha bado haujakamilika. Polisi
wa mpakani wapo hapa kila siku na watu wanaogopa
kuongea.
Wiki moja kamili kabla, Shawara aliondoka
nyumbani kwake kwa mara ya mwisho. Ndugu
yake, Daoud, aliondoka nyumbani kwake karibu
ya saa 1:30 kwa miguu, akielekea Umm Touba,
ambayo ipo ndani ya mipaka ya manispaa ya
Jerusalem, na ambapo wakati mwingine kazi
hupatikana katika ujenzi au Shambani. Daoud
anasimulia kwamba baada ya muda mfupi, jeep
ya Polisi wa mpakani ilitokea na kumkamata
yeye na wale vibarua wengine, jumla yao
wakiwa sita, ambao walikuwa wametoka hapo
kijijini. Hakuna hata mmoja wao aliyekuwa
na kibali cha kufanya kazi Israel. Sio muda
mrefu baadaye, Mahmoud akawasili pia, akiwa
amepanda nyumbu. Yeye pia alikuwa njiani
kwenda kutafuta kazi kama ilivyokuwa desturi
yake ya kila siku.
Wale Polisi wa mpakani walimuweka kizuizini
pia. Walinyang’anya kile kitambulisho
cha manjano cha kila mtu katika kikundi
hicho na wakawaamuru kwenda kituo cha Polisi
cha Talpiot, katika sehemu ya kusini ya
Jerusalem. Baada ya majadiliano kiasi, Daoud
anasema, wale Polisi wa mpakani waliwapeleka
huko kituoni kwa jeep yao. Mahmoud alikataa
kuingia kwenye jeep hiyo, akisema kwamba
asingeweza kumuacha yule nyumbu peke yake
pale peupe. Mabishano yakatokea, lakini
wale Polisi wa mpaka hawakutumia nguvu dhidi
ya Mahmoud, anasema ndugu yake Daoud. Daoud
alichukuliwa kwenye jeep na ndugu yake akabakia
pale na yule nyumbu na wale Polisi wa mpaka
waliobakia naye. Baada ya mahojiano mafupi
na baada ya kuweka saini ahadi ya kutoingia
tena Umm Touba, Daoud na wale wengine walipelekwa
kwenye kituo cha ukaguzi kipya cha Rachel
– kule kwenye kaburi la Rachel, karibu
na lango la kuingilia Bethelehem –
na wakatupwa kwenye njia yao.
Daoud hakumuona ndugu yake tena akiwa hai.
Akirudi kijijini karibuni saa 6:30 mchana,
hakuweza kumuona Mahmoud. Ni kijiji kidogo
cha watu 170, msiba mmoja hadi juma lililopita,
nyumba za mawe ukingoni mwa bonde la kustaajabisha
upande wa mashariki, makazi ya Har Homa
upande wa magharibi. Ni mabedui, watu wa
kabila la Taamra.
Saa 10 jioni Mohammed Hamadan alimuona yule
nyumbu anayekwenda shoti, akiacha vumbi
nyuma yake. Alikuwa anapita katika ile njia
ambayo inashuka kuelekea Umm Touba ambayo
imezungukwa pembeni na marundo ya takataka.
Sasa tunatembea katika ile njia kutoka Nuaman
kwenda Umm Touba, njia ambayo yule nyumbu
aliifuata angalau kwa sehemu yake tu. Ni
njia yenye mawe mawe. Mita mia chache tu
zinateganisha ile sehemu ambayo Shawara
alikamatwa na ile sehemu ambayo aligunduliwa
akiwa amefungwa kwenye nyumbu. Saa sita
na nusu zinatenganisha ule muda ambao kwamba
ndugu yake Shawara alimuona akiwa hai na
mzima na ule muda aliogunduliwa akiwa amefungwa
kwenye nyumbu. Hakuna anayejua ni nini kilichotokea
katika masaa yale.
Hamadan sasa anatafuta dalili za damu katika
ile njia iliyofuatwa na yule nyumbu, lakini
mvua kwa dhahiri ilikuwa imefuta kila kitu.
Hakuona majeraha katika mwili wa Mahmoud,
ni katika ule upande wa kushoto wa kichwa
chake uliopondwa tu. Alikuwa amefungwa kwenye
nyumbu kwa kamba ya nguo nyeusi. Hapa ndipo
pale alipomsimamisha yule Nyumbu, akizikamata
hatamu zake kwenye ule mteremko. Wafanyakazi
katika lile ghala la jirani la vifaa vya
ujenzi pia waliliona tukio hili. Mwenye
shughuli ile alikuwa ni Ahmed Abu Their,
ndiye aliyeita gari la wagonjwa. Yeye anasema
kwamba alimuona Mahmoud akiwa amefungwa
kwenye Nyumbu lakini aliogopa kusogelea.
Wanaume nyuso zao zikiwa na hofu, wamekaa
katika mgongo wa sehemu iliyoinuka na wanaisubiri
ile gari ya wagonjwa ilete ule mwili kutoka
Hadassar. Wanawake, katika mavazi meusi
wamekaa katika kivuli cha nyumba ya yule
mtu aliyekufa na wanaomboleza. Vijana wanapeperusha
bendera za Palestina katika mapaa ya nyumba
na katika wigo wa eneo la makaburi ambalo
liko chini ya kijiji hicho.
Msafara unakaribia kutoka kwenye bonde,
lile gari la wagonjwa la Wapalestina likiwa
mbele na taa nyekundu zimeweka mweka. Jeep
ya kijeshi ya Israeli inaangalia kwa mbali,
ikiwa imesimama kwenye barabara ya usalama
iliyotiwa kibamba sambamba na ule ukuta
unaotenganisha ambao unajengwa kama kinga
ya Jerusalem. Hakuna hata mmoja hapo kijijini
anayejua ulipo mpaka kati ya maeneo hayo
na Jerusalem. Hapo ukuta huo utakapokamilika
yote yatakuwa wazi. Hapo Nuaman ni mkazi
mmoja tu aliye na kitambulisho cha kadi
ya buluu cha Jerusalem, kila mtu mwingineo
ni kitambulisho cha “Maeneo.”
Jirani ya Umm Touba ni Jerusalem lakini
sio wakazi wote wenye kadi za buluu. Mtu
mmoja karibu yangu anafuta chozi. Mwili
unatolewa kwenye gari la wagonjwa kuingizwa
ndani ya nyumba. Huko ndani uso wa marehemu
unafunuliwa, uso wa mkulima mdogo, ulio
na sharubu ndefu, uliojeruhiwa – na
mara unafunikwa haraka.
Mwanasheria wa kijiji, Daoud Darawi, anayefanyakazi
katika tawi la Palestina la Ulinzi kwa watoto
kimataifa (DCI) Ramallah, anadai uchunguzi
wa kimataifa juu ya mazingira ya kifo cha
Shawara. “Walimfanyia yeye kile wazungu
walichowafanyia wahindi huko marekani,”
anasema. Anaelezea juu ya masuala mawili
kama hayo. Katika kijiji cha karibu cha
Dar Salah, Polisi wa mpakani wakiwa ndani
ya jeep walimshambulia punda ambaye juu
yake alikuwa amepanda Walid Amiya, wakimuangusha
chini. Alinusurika. Katika kijiji cha karibu
cha Wadi al-Humos walimfunga Maamoun Abu
Ali kwenye punda wake na wakajaribu kumfukuzia
kwenye njia yake mnyama huyo. Yeye pia alinusurika.
(Tutamrudia baadaye).
Kwa mujibu wa wakili Darawi, hao Polisi
wa mpakani wamekuwa hapo kwa takriban mwezi
mmoja. Tangu kuwasili kwao, matukio ya kuwatesa
vibarua wanaotafuta kazi katika kijiji cha
jirani yamezidi. ‘Njoo siku moja majira
ya saa 11 asubuhi na utaona ni nini kinachotokea
hapa kila siku na hawa Polisi wa mpakani,’
mwanasheria huyo anasema. Familia ya Mahmoud
Shawara iliandikisha malalamiko kwenye Idara
ya upelelezi ya Polisi (PID).
Msemaji wa Wizara ya Sheria, Yaacor Galant,
alisema wiki iliyopita kwa niaba ya PID:
‘Uchunguzi wetu mzuri sana, ambao
tumeufanya kuanzia pale malalamiko haya
yalipopokelewa mpaka Ijumaa iliyopita, wakati
wa mchana, unaonyesha kwamba hakuna uhusiano
kati ya shughuli za Polisi wa mpakani na
kuumia na kufa kwa mtu huyu. Ni dhahiri
kwamba alionywa kuhusu nyumbu huyo, akaambiwa
asimpande. Alikuwa ni nyumbu wa porini.
Ni dhahiri kwamba alimpanda, akamuendesha
na pia akajifunga mwenyewe kwenye nyumbu
huyo.’ Je, uchunguzi umekamilishwa
sawasawa? Gallant aliahidi kufuatilia na
kurejea kwangu muda mfupi baadaye. Kwa wakati
huu hakuna lolote jipya.
Hatujapata ushahidi utakaohusisha polisi
wa mpakani (na tukio hili). Tutafurahi kupokea
ushahidi mwingine. Kwa wakati huu hakuna
anayeweza kuelekeza kwenye uhusiano makhsusi
baina ya Polisi wa mpakani na suala hili.
Maamoun Abu Ali ni mfanyakazi wa ujenzi
katika jengo ambalo linapanda katika ujirani
wa Doha katika sehemu ya kusini ya Bathelehemu.
Tulimfuata Jumanne ya wiki hii. Kapera mcheshi
wa miaka 20, alikuwa bado anayo makovu ya
mapambano yake na Polisi wa mpakani katika
lile bonde chini ya Nuaman. Abu Ali anatoka
kwenye kijiji cha jirani cha Abadiya. Kama
miezi miwili iliyopita, wakati wa Ramadhani,
alikuwa amempanda punda wake akiwa njiani
kuelekea kijiji cha karibu cha Wadi Humos
kununua kuku kwa ajili ya kifungua kinywa
kwenye duka la nyama la Shahar. Ilikuwa
ni muda kidogo baada kuingia adhuhuri. Mara
jeep ya polisi wa mpakani ikasimama karibu
yake. “Unakwenda wapi?” Abu
Ali aliulizwa, na yeye akajibu; “Nakwenda
kununua kuku.” Polisi wa mpakani akakagua
vile vitu ambavyo punda alikuwa amebeba
halafu akachunguza makaratasi ya Abu Ali,
Shabah, na Bingo.
Kwa zile hatamu za mnyama huyo wakamfunga
mikono Abu Ali nyuma ya mgongo wake na wakamfanya
alalie tumbo lake juu ya ardhi, uso chini.
Polisi wa mpakani wanapenda kuwaadhibu shabahim
wanaowakamata. Abu Ali anasimulia kwamba
walimfunga kipande cha gogo la mkaa mgongoni
mwake kisha wakamchapa yule mnyama kumfanya
atembee. Punda wa Abu Ali ni mzee na ni
mbishi, au labda anamtii bwana wake tu –
vyovyote iwavyo, alikataa kusogea. Abu Ali
anasema yeye pia alivuta kwa mikono yake
iliyofungwa ili punda huyo asisogee. Sio
vigumu kukisia ni ini kingetokea kama punda
huyo angebabaika na kuanza kwenda shoti,
na Abu Ali alikuwa amelala uso chini, mikono
imefungwa mgongoni kwake mnyama huyo. Wakati
mmoja Polisi wa mpakani pia alisimama mgongoni
mwa Abu Ali, mguu mmoja juu yake na mwingine
kwenye kigogo cha mkaa, ili kumbana.
Unyanyasaji uliendelea kwa takriban robo
saa, Abu Ali anasema. Hatimaye wale Polisi
wa Israeli walikata tamaa kumfanya yule
punda mbishi asogee na wakamuamuru Abu Ali
kusimama. Waliongea Kiarabu. Abu Ali anasema
kwamba mmoja wao alimfunika macho yake kwa
mikono yake na yule mwingine akampiga mara
moja usoni mwake kwa jiwe. Bado ana kovu
upande wa kulia, chini ya mdomo wake. Walimtishia
wakimwambia kwamba kama angezurura hapo
tena atauawa. Kisha wakamuelekeza kwenye
njia yake. Abu Ali hakusajili mashtaka kwenye
Idara ya upelelezi ya Polisi. Alitaka alalamike
kwa Polisi wa Palestina halafu wao wayafikishe
malalamiko hayo lakini alishauriwa kutokufanya
hivyo na Polisi mmoja wa kijiji chake, ambaye
alimwambia: ‘Watu wanauawa hapa, hivyo
shukuru kwamba uko hai na mwenye afya.’
Wacha tuuambie ulimwengu kwamba kile wanachotufanyia
sisi, kuhusu yale maisha ya karaha ya kumilikiwa
kiharamu, Mzee Mohammed Abu Ranar Adum,
mmoja wa wakuu wa kijiji hiki anasema katika
maneno yake ya kusifia. Mazishi yanakaribia
kutawanyika kimya kimya. Katika kivuli cha
mizeituni, ukingoni mwa kijiji hiki, kando
ya bonde, amesimama nyumbu, aliyefungwa
kwenye mti. Mnyama wa rangi ya hudhurungi
mwenye nguvu. Tunaposogelea kuchukua picha
yake, nyumbu huyo anaonyesha dalili ya kutaharuki,
anageuza kichwa chake upande na anajaribu
bila mafanikio kujifungulia kuwa huru.
Mwandishi wa makala hii ni
Gideon Levy wa Haarez
|